MASOMO JUMAMOSI JUMA LA 30 LA MWAKA KUMBUKUMBU YA MT.KAROLI BOROMEO

SOMO 1:Rum.11:1-2,11-12,25-29

Nauliza. Je! Mungu aliwasukumia mbali watu wake? Hasha! Kwa kuwa mimi nami ni Mwisraeli, mmoja wa wazao wa Ibrahimu, mtu wa kabila ya Benyamini. Mungu hakuwasukumia mbali watu wake aliowajua tokea awali.
Basi nasema, Je! Wamejikwaa hata waanguke kabisa? Hasha! Lakini kwa kosa lao wokovu umewafikilia Mataifa, ili wao wenyewe watiwe wivu. Basi, ikiwa kosa lao limekuwa utajiri wa ulimwengu, na upungufu wao umekuwa utajiri wa Mataifa, je! Si Zaidi sana utimilifu wao?
Kwa maana, ndugu zangu, sipendi msiijue siri hii, ili msijione kuwa wenye akili; ya kwamba kwa sehemu ugumu umewapata Israeli, mpaka utimilifu wa Mataifa uwasili. Hivyo Israeli wote wataokoka; kama ilivyoandikwa, Mwokozi atakuja kutoka Sayuni; Atamtenga Yakobo na maasia yakee. Na hili ndilo agano langu nao, Nitakapowaondolea dhambi zao.
Basi kwa habari ya Injili wamekuwa adui kwa ajili yenu; bali kwa habari ya kule kuchaguliwa wamekuwa wapenzi kwa ajili ya baba zetu. Kwa sababu karama za Mungu hazina majuto, wala mwito wake.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 94:12-15,17-18 (K) 16

(K) Bwana hatawatupa watu wake.

Ee Bwana, heri mtu yule umwadhibuye,
Na kumfundisha kwa sheria yako;
Upate kustarehesha siku za mabaya,
Hata asiye haki atakapochimbiwa shimo. (K)

Kwa kuwa Bwana hatawatupa watu wake,
Wala hutauacha urithi wake,
Maana hukumu itairejea haki,
Na wote walio wanyofu wa moyo wataifuata. (K)

Kama Bwana asingalikuwa msaada wangu,
Nafsi yangu kwa upesi ingalikaa penye kimya.
Niliposema, Mguu wangu unateleza;
Ee Bwana, fadhili zako zilinitegemeza. (K)

SHANGILIO
Zab. 119:135

Aleluya, aleluya,
Umwangazie mtumishi wako uso wako, na kunifundisha amri zako.
Aleluya.


INJILI:Lk.14:1,7-11

Yesu alipoingia ndani ya nyumba ya mtu mmoja miongoni mwa wakuu wa Mafarisayo siku ya sabato, ale chakula, walikuwa wakimvizia.
Akawaambia mfano wale walioalikwa, alipoona jinsi walivyochagua viti vya mbele; akisema, Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele Zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe. Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.

No comments:

Powered by Blogger.