MASOMO JUMA LA 27 LA MWAKA JUMATATU 9 0KTOBA 2017

SOMO 1:Yon.1:17;2:10

Neno la Bwana lilimjia Yona, mwana wa Amitai, kusema, Ondoka, uende Ninawi, mji ule mkubwa, ukapige kelele juu yake; kwa maana uovu wao umepanda juu mbele zangu. Lakini Yona akaondoka akimbilie Tarshishi, apate kujiepusha na uso wa Bwana; akatelemka hata Yafa, akaona merikebu inayokwenda Tarshishi; basi, akatoa nauli, akapanda merikebuni, aende pamoja nao Tarshishi, ajiepushe na uso wa Bwana. Lakini Bwana alituma upepo mkuu baharini, ikawa tufani kubwa baharini, hata merikebu ikawa karibu na kuvunjika.
Basi wale mabaharia wakaogopa, kila mtu akamwomba mungu wake; nao wakatupa baharini shehena iliyokuwa merikebuni, ili kuupunguza uzito wake. Lakini Yona alikuwa ameshuka hata pande za ndani za merikebu; akajilaza, akapata usingizi. Basi nahodha akamwendea, akamwambia, Una nini Ewe ulalaye usingizi? Amka, ukamwombe Mungu wako; labda Mungu huyo atatukumbuka, tusipotee.
Wakasemezana kila mtu na mwenzake, Haya, na tupige kura, tupate kujua mabaya haya yametupata kwa sababu ya nani. Basi wakapiga kura, nayo kura ikamwangukia Yona. Ndipo wakamwambia, Tafadhali utuambie, wewe ambaye mabaya haya yametupata kwa sababu yako; kazi yako ni kazi gani? Nawe umetoka wapi? Nchi yako ni nchi ipi? Nawe u mtu wa kabila gani? Akawaambia, Mimi ni Mwebrania, nami namcha Bwana, Mungu wa mbingu, aliyeviumba bahari nan chi kavu.
Ndipo watu wale wakaogopa mno, wakamwambia, Ni jambo gani hili ulilolitenda! Kwa maana watu wale walijua ya kuwa amekimbia, ajiepushe na uso wa Bwana, kwa sababu alikuwa amewajulisha. Basi wakamwambia, Tukutende nini, ili bahari itutulilie? Kwa maana bahari ilikuwa inazidi kuchafuka. Naye akawaambia, Nikamateni, mnitupe baharini; basi bahari itawatulilia; kwa maana najua ya kuwa ni kwa ajili yangu tufani hii imewapata. Lakini wale watu wakavuta makasia kwa nguvu, ili wapate kurudi pwani, wasiweze; kwa maana bahari ilizidi kuwachafukia sana.
Basi wakamlilia Bwana, wakasema, Twakuomba, Ee Bwana, twakuomba, tusiangamie kwa ajili kwa ajili ya uhai wa mtu huyu, wala usitupatilize kwa ajili ya damu isiyo na hatia; kwa maana wewe, Bwana, umefanya kama ulivyopenda. Basi wakamkamata Yona, wakamtupa baharini, nayo bahari ikaacha kuchafuka. Ndipo wale watu wakamwogopa Bwana mno, wakamtolea Bwana sadaka, na kuweka nadhiri.
Bwana akaweka tayari samaki mkubwa ili ammeze Yona, naye Yona akawa ndani ya tumbo la samaki yule muda wa siku tatu, mchana na usiku. Bwana akasema na yule samaki, naye akamtapika Yona pwani.


WIMBO WA KATIKATI
Yon. 2:1-3, 7 (K) 6
(K) Umenipandisha nafsi yangu kutoka shimoni. Ee Bwana.

Nalimlilia Bwana kwa sababu ya shida yangu,
Naye akaniitikia;
Katika tumbo la kuzimu naliomba,
Nawe ukasikia sauti yangu. (K)

Maana ulinitupa vilindini,
Ndani ya moyo wa bahari;
Gharika ya maji ikanizunguka pande zote;
Mawimbi yako yote na gharika zako zote
Zimepita juu yangu. (K)

Nami nikasema, Nimetupwa mbali na macho yako;
Lakini nitatazama tena kukabili hekalu lako takatifu. (K)

Roho yangu ilipozimia ndani yangu.
Nalimkumbuka Bwana;
Maombi yangu yakakuwasilia.
Katika hekalu lako takatifu. (K)

SHANGILIO
Yn. 17:17

Aleluya, aleluya,
Neno lako ndiyo kweli, Ee Bwana ututakase kwa ile kweli.
Aleluya.

INJILI:Lk.10:25-37

Mwana-sheria mmoja alisimama akamjaribu Yesu, akisema, Mwalimu, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele? Akamwambia, Imeandikwa nini katika torati? Wasomaje? Akajibu akasema, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zote; na jirani yako kama nafsi yako. Akamwambia, Umejibu vema; fanya hivi nawe utaishi.
Naye akitaka kujidai haki, alimwuliza Yesu, Na jirani yangu ni nani? Yesu akajibu akasema, Mtu mmoja alishuka toka Yerusalemu kwenda Yeriko, akaangukia kati ya wanyang’anyi; wakamvua nguo, wakamtia jeraha, wakaenda zao, wakimwacha karibu ya kufa. Kwa nasibu kuhani mmoja alishuka kwa njia ile; na alipomwona alipitia kando. Na Mlawi vivyo hivyo, alipofika pale akamwona, akapitia kando.
Lakini, Msamaria mmoja katika kusafiri kwake alifika hapo alipo; na lipomwona alimhurumia, akakaribia, akamfunga jeraha zake, akizitia mafuta na divai; akampandisha juu ya mnyama wake, akampeleka mpaka nyumba ya wageni, akamtunza. Hata siku ya pili akatoa dinari mbili, akampa mwenye nyumba ya wageni, akisema, Mtunze huyu, na chochote utakachogharimiwa Zaidi, mimi nitakaporudi nitakulipa.
Waonaje wewe, katika hao watatu, ni yupi aliyekuwa jirani yake, yule aliyeangukia kati ya wanyang’anyi? Akasema, Ni huyo aliyemwonea huruma. Yesu akamwambia, Enenda zako, nawe ukafanye vivyo hivyo.

No comments:

Powered by Blogger.