MASOMO YA MISA JUMA LA 28 LA MWAKA JUMAMOSI 21 OKTOBA 2017

SOMO 1:Rum.4:13,16-18

Ahadi ile ya kwamba atakuwa mrithi wa ulimwengu alipewa Ibrahimu na uzao wake si kwa sheria bali kwa haki aliyohesabiwa kwa Imani. Kwa hiyo ilitoka katika Imani, iwe kwa njia ya neema, ili kwamba ile ahadi iwe imara kwa wazao wote; si kwa wale wa torati tu, ila na kwa wale wa Imani ya Ibrahimu; aliye baba yetu sisi sote; mbele zake yeye aliyemwamini, yaani Mungu, mwenye kuwahuisha wafu, ayatajaye yale yasiyokuwako kana kwamba yamekuwako.
Naye aliamini kwa kutarajia yasiyoweza kutarajiwa, ilia pate kuwa baba wa mataifa mengi, kama ilivyonenwa, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 105:6-9, 42-43 (K)

(K) Bwana analikumbuka agano lake milele.

Enyi wazao wa Ibrahimu, mtumishi wake;
Enyi wana wa Yakobo, wateule wake.
Yeye, Bwana, ndiye Mungu wetu;
Duniani mwote mna hukumu zake. (K)

Analikumbuka agano lake milele;
Neno lile aliloviamuru vizazi elfu.
Agano alilofanya na Ibrahimu,
Na uapo wake kwa Isaka (K)

Maana alilikumbuka neno lake takatifu,
Na Ibrahimu, mtumishi wake.
Akawatoa watu wake kwa shangwe,
Na wateule wake kwa nyimbo za furaha. (K)


SHANGILIO
Mt. 4:4

Aleluya, aleluya,
Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.
Aleluya.

INJILI:Lk.12:8-12


Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Nami nawaambia, kila atakayenikiri mbele ya watu, Mwana wa Adamu naye atamkiri yeye mbele ya malaika wa Mungu; na mwenye kunikana mbele ya watu, huyo atakanwa mbele ya malaika wa Mungu.
Na kila mtu atakayenena neno juu ya Mwana wa Adamu atasamehewa, bali aliyemkufura Roho Mtakatifu hatasamehewa.
Na watakapowapeleka ninyi mbele ya masinagogi na maliwali na wenye mamlaka, msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu jinsi mtakavyojibu au kusema; kwa kuwa Roho Mtakatifu atawafundisha saa ile ile yawapasayo kuyasema.

No comments:

Powered by Blogger.